Sehemu ya pili
______________________
Neno "mocumentary"
ambalo linabeba jina la album yake ya tatu, ambalo Jay Moe
hulitamka kama "mokyumenari" limetokana na muunganiko wa maneno
Jay Moe na Documentary. Utaratibu huu wa kuunganisha maneno
wanamofolojia wa kiingereza huuita "Blending" ambapo sehemu ya
neno moja huunganishwa na sehemu ya neno lingine kutengeneza
neno jipya. Kwenye neno Jay moe amechukua Mo na kwenye neno
Documentary amechukua Cumentary, akayaunganisha ikawa mocumentary.
Kwa maneno rahisi waweza sema "Mocumentary" ni Documentary za
jay moe au Makala za Juma Mchopanga.
Jay moe
anatukumbusha kwamba yupo katika game kabla ukumbi wa Diamond
Jubilee haujaanza kujazwa kwa maonesho ya wasanii mwanzoni mwa
miaka ya 2000. Diamond Jubilee kwa mara ya kwanza ilijazwa na
Juma Nature katika uzinduzi wa album ya Ugali mwaka 2003
(Mkoloni, 2016). Mdau mmoja alishawahi kusema "Juma Nature ni msanii
pekee aliyewahi kuijaza diamond jubilee mara tatu na watu wakakosa
pakukanyaga". Leo hii msanii kuujaza ukumbi mdogo tu wa
maisha club, billz n.k anaandaa msululu wa wasanii ili kumpa
sapoti kwenye shoo yake na bado ukumbi unaweza usijae.
Ukiacha Juma Nature Diamond jubilee iliwahi kujazwa wasanii
wengine kama Profesa Jay, Daz nundaz, Gangwe Mobb, Dully sykes
na T.I.D katika uzinduzi wa pamoja wa albam zao n.k (Ngwesa
& Palla, 2016).
Ni enzi hizo pia Jay moe anasema
nyimbo zilikuwa hazirekodiwi kwa kompyuta katika studio nyingi
kama sasa. G solo katika kitabu chake kiitwacho harakati za
Bongo Fleva anasema kwamba “Studio za kwanza ambazo
zilikuwa ni analogy (analojia) zilimikiwa na watu
binafsi waliokuwa ndugu na zilikuwa eneo la Magomeni
Mikumi na zote zilikuwa katika nyumba moja.
Wamiliki hao ambao ni Paul Muuto na mdogo wake
Gerry Gumbo. Walikuja kuziuza studio hizo kwa taasisi
za Don Bosco ndipo ikazaliwa Don Bosco Studio
mwaka 1992. Mnamo mwaka 1994 studio ya mawingu
ilianza kazi rasmi…. Mwaka 1998 MJ records ilianzishwa
ikimilikiwa na Master J... studio moja tu ndiyo
ilitumia mfumo wa digital (dijitali) ambayo ni
sound crafters. Bei za kurekodi studio za analogy
ilikuwa ni Shilingi 8,000 na kwenye studio zilizokuwa
digital ilikuwa shilingi 25,000” (Mwanjoka, 2011).
Wakati Jay Moe anaingia katika ulingo wa muziki wa Tanzania,
ni wakati ambao muziki wa Tanzania ulikuwa umetawaliwa na muziki
wa Taarabu na Dansi/Bolingo na ndio ulikuwa ukipewa nafasi
kubwa katika vyombo vya habari kuliko muziki wa kizazi kipya.
Wenye kumbukumbu nzuri mtakumbuka katika kipindi hicho kuelekea
mwishoni mwa miaka ya 90 na mwanzoni mwa miaka ya 2000 ndipo
kulikuwa na ushindani katika muziki wa Taarabu kati ya
Khadija Kopa na Nasma Khamis Kidogo hali iliyepelekea kuanzia
mtindo wa “mipasho” katika muziki wa taarabu kutokana na
kutupiana vijembe katika nyimbo.
Ikumbukwe nyakati hizi
ndizo nyimbo maarufu kama ‘Mambo iko huku”, “Sanamu la Michelin”
za Nasma Kidogo, “Kinyago cha Mpapure” ya Mwanahawa Ally n.k
zilikuwa zimeshika chati hali iliyofanya baadhi ya waimbaji
taarabu kushirikishwa na wanamuziki wa kizazi kipya kwa mfano
marehemu Nasma aliwahi kushikishwa katika kibao cha Gangwe Mobb
kiitwacho wape Vidonge vyao. Abdul misambano pia alishawahi
kushirikishwa kuimba kiitikio cha ‘asu’.
Katika muziki wa
dansi, hiki kilikuwa kipindi ambacho bendi ya African Stars
ama Twanga Pepeta ilikuwa katika ubora wake bila kuwasahau Tamtam,
TOT, Wajelajela (ndanda Kosovo), Msondo Ngoma n.k walikuwepo pia
katika chati. Twanga pepeta ilitawala muziki wa Tanzania kwa
vipindi vikuu viwili kwa kipindi hicho; wakati safu ya uimbaji
ikiongozwa na Banza stone aliyejiunga na Twanga mwaka 1995 na
kutamba na nyimbo kama “kisa cha mpemba” n.k. Banza alipoondoka
twanga mwaka 2001, Ally choki akashika usukani na kutamba na
vibao kama ‘Jirani’, ‘chuki binafsi’ n.k. Upande mwingine
Muumini mwinjuma alikuwa yuko moto na bendi ya Tamtam huku akipata
umaarufu na kibao chake cha “Tunda”.
Kipindi hiki pia
utaona waimbaji wa muziki wa dansi walianza kushirikishwa na
wasanii wa muziki wa kizazi kipya. Wenye kumbukumbu mnaukumbuka
wimbo wa “Achana nao” wa Mad Brain na Sister P wakimshirisha
Ally Choki kuimba kiitikio cha wimbo huo. Tusiusahau pia wimbo
wa “Msafiri” wa Kwanza Unit ambao walimshirikisha mzee wetu
King Kikii (Mzee sugu au mzee wa kitambaa cheupe), “Hapo
zamani” ya Sugu ft King Kiki na Kuna msanii (Nimemsahau jina)
aliwahi kutumia kiitikio cha “Napenda Nipate lau nafasi” ya
Kilwa Jazz Band. Huu wimbo wa msafiri humo ndani King Kikii
hakushirikishwa tu bali Master Jay (mtayarishaji wa kibao hicho)
alisampo kibao hicho pia. Kuna uwezekano hiki kikawa ndio kibao
cha kwanza cha muziki wa dansi Tanzania kusampuliwa na
watayarishaji wa muziki wa kizazi kipya.
Asha Baraka,
mkurugenzi wa bendi ya Twanga Pepeta anakubaliana na Jay Moe
anaposema kwamba mziki wa kizazi ndio chanzo cha kufa (kuzorota)
kwa taarabu na bolingo (dansi). Katika mahojiano na Gazeti la
Mwananchi aliwahi kunukuliwa akisema ukuaji wa muziki wa kizazi
kipya umeathiri soko la dansi. Anasema mwanzoni mwitikio
ulikuwa mkubwa kuliko sasa hata mchango wa vyombo vya habari
umepungua upande wa kupiga nyimbo za dansi hewani (Matandiko, 2014).
Itaendelea...........
Imeandikwa na
MALLE HANZI
0715076444
©2016
Powered by @babalaoTV www.babalaoinc.blogspot.com
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
-
❝BABU MWENYE NYUMBA❞ {♡Love Story♡_____Part..19} ∪₥ri_____+ ℳtunzi: ₲eofrey Mustafa, ₳rtist Jafa ✍ ℳaahali: Dar es salaam🇹🇿 ₩ha...
-
❝BABU MWENYE NYUMBA❞ {♡Love Story♡_____Part..29} ∪₥ri_____+ ℳtunzi: ₲eofrey Mustafa, ₳rtist Jafa ✍ ℳaahali: Dar es salaam🇹🇿 ₩ha...
-
❝BABU MWENYE NYUMBA❞ {♡Love Story♡_____Part..26} ∪₥ri_____+ ℳtunzi: ₲eofrey Mustafa, ₳rtist Jafa ✍ ℳaahali: Dar es salaam🇹🇿 ₩h...
No comments:
Post a Comment