Wednesday, December 30, 2015

NIKKI MBISHI AAMUA KUFATA NYAYO ZA WEUSI [WWW.BABALAOINC.BLOGSPOT.COM]

NANUKUU
Kabla ya mimi na yeye kuwa chini ya Tamadunimuzik iliyoanza mwaka 2011; Nikki mbishi ni msanii ambaye nimeanza kumsikia baada ya miaka ya 2000 kugawanyika. Uwezo wake wa kisanaa sio kitu ambacho napaswa kubishania, itoshe tu kusema jamaa anajua. Najua anatambua uwezo wangu katika uandishi na ndiye aliyethubutu kunipachika jina la "Nyambari Nyangwine" japo sikuwahi kulipenda lakini watanzania wakiamua wameamua.
Nidiklee interesti kwamba Mimi na Nikki tunafahamiana na tumewahi na tunafanya kazi pamoja kama Tamadunimuzik japo kuna baadhi ya mambo ya muziki nimeyaweka kando lakini ntaendelea kuwa sehemu ya Tamadunimuzik kwa kadri nitakavyobarikiwa. Kwa hivyo makala hii haitaegemea upande wowote kama ambavyo nilifanya makala iliyomhusu Bonta japo baadhi yenu mliishutumu Tamadunimuzik lakini makala hii na zijazo zibakie kuheshimiwa kama mawazo yangu peke yangu na sio ya kikundi chochote.
Mwaka jana mwezi kama huu niliwahi kuweka "Post" katika mtandao wa jamii nikisema kuwa wakati mwaka 2014 ukiwa unaelekea kufikia tamati wasanii Nikki Mbishi na One the incredible walipewa ushauri na ndugu Fredrick Bundala maarufu kama Sky Walker ambaye ni mhariri wa Bongo 5 kuwa wakitaka kufanikiwa hawana budi kufanya kile ambacho kundi la Weusi wamefanya mpaka wamefikia hapo walipo. Ama kwa Lugha nyingine Nikki Mbishi afuate nyayo za weusi ili afanikiwe.
Katika makala hii nitamzungumzia zaidi Nikki Mbishi japo makala ile ya ndugu Fredrick Bundala (Sky Walker) ambaye katika makala hii nitatumia jina “Mwandishi” kumwakilisha ilikuwa imeandikwa kuwalenga watu wawili yaani Nikki Mbishi na One the Incredible. Nitafanya hivyo kwa sababu haya nitakayoyajadili yanamhusu zaidi Nikki Kuliko One the Incredible. Kwa ambao hamkuwahi kuisoma makala hiyo inapatikana katika tovuti ya Bongo5 ikiwa na kichwa cha habari “Kwanini Nikki Mbishi na One The Incredible wanapaswa kujifunza kutoka kwa Weusi”.
Kumwambia Nikki Mbishi afuate njia ambazo weusi wamepitia ili afanikiwe kimuziki ilikuwa kumkejeli. Sababu kubwa ni kwamba wakati ushauri unatoka ndio wakati ambao Nikki Mbishi alikuwa na Mgogoro mkubwa na Weusi hivyo ingewezekanaje umwambie awe kama watu ambao ana mgogoro nao. Naamini ndio ulikuwa wakati muafaka ambao Nikki mbishi alikuwa akiamini amemaliza changamoto anaweza “ku –create enemity” na isimuathiri kisanaa tofauti na alivyoamini katika kibao chake cha “Punchline”.
Mwandishi anaweza pia kuwa sahihi kwa sababu Nikki alishawahi kusema kwamba yeye hajakamilika “sometime anakosea, msije mkahamasika mkamuiga na kupotea”. Hilo linawezekana kabisa ndani ya kizazi hiki ambacho “kinakua kinaona na kusikia, kudadisi, kujaribu na mwisho kutumbukia”. Yote kwa yote Nikki mbishi ni Mc ambaye anaamini katika nyayo zake sio nyayo za mtu mwingine ili kupata mafanikio. Alishawahi kusema “andagraundi wanawishi kwa kila hali na mali, wakifata nyayo (zake) hakika watafika mbali”. Sasa kama wanaofata nyayo zake wanaweza kufika mbali vipi mwenye nyayo ashindwe kufika mbali.
Mwandishi alishawahi pia kueleza chanzo cha Mgogoro wa Nikki na Memba wa weusi kimojawapo ni Jina “Nikki” ndio kukawepo Tension kati ya Nikki Mbishi na Nikki wa Pili (Bundala, 2012). Sijui ndio kisa Nikki Mbishi kuuliza “Kivipi Nikki wa pili wa kwanza hajulikani?” na labda ndio kilichomchochea Raf Mc wa utengwani kusema “(a)nawachana wote manikki wawili”
Mwandishi anaendelea kueleza kwamba mstari huo wa kuhoji kivip nikki wa kwanza hajulikani? Ndicho kilichopelekea Rama D ambaye alikuwa ameshirikishwa na Nikki Mbishi kuimba kiitikio cha wimbo wa Punchline kuomba sauti zake ziondolewe katika kibao hicho kwakuwa hakutaka kugombana na Joh Makini ambaye inasemekana hakuwa akimpenda Nikki Mbishi. Hivyo ndio baadaye Grace Matata akaimba kiitikio cha wimbo huo (Bundala, 2012).
Hii inanikumbusha kisa nilichowahi kukisikia kwamba, mgogoro wa Nikki na Weusi ulichochewa zaidi na shoo moja ya Dar Live. Katika shoo hiyo Nikki alihudhuria kama mtazamaji na wasanii wengine waliokuwepo ni baadhi memba wa weusi na Fid Q. Fid Q alipopanda jukwaani alimuita Nikki mbishi katika jukwaa kumpa tafu. Kitendo hiko hakikuwapendeza mmoja kati ya memba wa weusi hali iliyomfanya kutoa maneno ambayo yalipokuja kumfikia Nikki Mbishi hayakumpendeza.
Mwandishi alionesha yuko “Fair” mwanzoni mwa makala yake kwa kutambua uwezo wa Nikki Mbishi kwa kusema anamkubali, hana mpinzani katika Mitindo huru na pia japo yeye amepitia maisha ya kuandika mistari lakini hawezi kufikia hata robo ya uwezo wa Nikki (Bundala, 2014). Kama unazikumbuka nyimbo za Sky Walker alizotoa hasa kipindi anatangaza Radio Free Africa (RFA) unaweza kukubaliana ama kutokubaliana kauli yake hiyo.
Kabla ya makala hiyo ya mwandishi, Nikki Mbishi alishawahi kusema kwamba “(yuko) kwenye Mainstream ya Underground” yaani kwa kiswahili rahisi ni kwamba “yuko kwenye mkondo mkuu wa Hip Hop ya handakini (Underground Hip Hop)”. Kwa mujibu wa mwandishi anasema Underground Hip Hop ni Hip Hop ambayo iko nje ya mfumo wa biashara kwa sababu hujiusisha na uandishi wa mashairi Conscious yaliyo chanya na yasiyo ya kibiashara (Bundala, 2014).
Nikki alishasema kwanza “kufunza ndo kazi yangu na mziki kwangu ni ajira”. Mziki huo wa Underground Hip Hop ndio ambao Nikki aliamini ndio ajira yake lakini mwandishi alimshauri kwamba kufanya Underground ni kupoteza muda tu kama anafanya muziki kupata chochote labda kama anafanya kujifurahisha tu. Underground Hip Hop haivutii mkondo mkuu wa biashara itaishia kumpa sifa tu. Kibongobongo mashabiki hawanunui kazi za Underground tofauti na mbele ambapo wasanii wa aina hiyo ya muziki wana maisha mazuri kwa sababu mashabiki wananunua kazi (Ibid).
Mwandishi alitamani Nikki afanikiwe kama Weusi alitamani kuona siku moja akipost picha katika mitandao ya kijamii akiwa airport akiwa anawahi shoo za mikoani kama wanavyoweka weusi hasa hasa Joh Makini. Si unajua mambo ya ku-post “Mwanza..niko njiani nakuja… tukutane Rock Bottom” huku picha ikisindikizwa na selfie akiwa kwenye kiti cha ndege huku mpiga picha akihakikisha dirisha duara linaonekana. Msanii gani hapendi…??
Nikki alijipambanua daima kama msanii “fanisi mwenye fikra yabisi” lakini mwandishi alimshauri kukubali mabadiliko katika Hip Hop asiwe mhafidhina (conservative) hata kwenye mdundo wa kapuka anaweza kuchana. Nadhani hilo limejibiwa juzi katika wimbo wake uitwao ‘Indebe’ ambapo katika wimbo huo anasema “wengine wana-judge jinsi navyobadilika”. Kumbe Nikki Mbishi anajua kuwa anabadilika? Unaweza kujiuliza ni nini? Lakini katika ubeti wa pili mwishoni anakujibu kuwa anajua kuwa “wengine wanakatwa mizuka, eti kisa… amefanya kapuka”. Kwa hivyo nikki kachana kwenye biti ya kapuka kama Sky Walker alivyoshauri.
Nikki pia alishauriwa na mwandishi kuchagua midundo mizuri na kuachana midundo migumu kwa sababu zinasikika kama za miaka ya 90 ambazo ni za kizamani na zisizo rafiki masikioni mwa mashabiki ambao hawana uelewa na beat hizo ngumu. Mwandishi kwa kujua kwamba Duke Tachez na Watayarisha midundo wa Tamadunimuzik wamejikita katika utayarishaji wa midundo ‘Underground Hip Hop’ ambayo yeye hataki Nikki aendelee kutumia akashauri Nikki ni Lazima afanye kazi na watayarishaji wengine nje ya Tamadunimuzik.
Nikki ameufanyia kazi ushauri huo japo ni kweli hii sio mara ya kwanza kufanya na maprodyuza wengine ama katika midundo ambayo sio ya Boom Bap. Kabla ya kuwa Mlab wenye kumbukumbu nzuri mtakumbuka alishawahi kufanya Ngoma ziitwazo “Kichaa cha Mbwa” na “Things Fall Apart”. Baada ya ushauri huo kutoka kwa Sky Walker ni kama Nikki ameamua kuusikiliza au kaamua kwa maamuzi yake mwenyewe kufanya nyimbo ambazo haziko katika mahadhi ambayo tumemzoea. Nikki katika mixtape yake ya hivi karibuni “Ufunuo wa Unju Bin Unuq” amefanya nyimbo kama Tulia (R&B beat), Unachonipendea (Dance Hall Beat), Indebe (Kapuka Beat) na Tembo (Afro Beat).
Lakini pia mkumbuke ameshawahi kufanya kolabo katika wimbo wa ‘Joto Hasira’ na hivi karibuni kashirikishwa na Pinda bway katika kibao kiitwacho ‘Turn Up The Music’ ambazo zote sio midundo ya Hip Hop. Huyu Nikki wa sasa ni tofauti na yule ambaye halikuwa anachagua midundo ya kuchania sitaki kusema ameamua kuufata ushauri wa mwandishi. Pia sitaki kusema kuwa Nikki mbishi anatakiwa kuufata ushauri ila auzingatie wa Nash Mc kwamba Beat za Baibuda, kiduku, za kinaijeria vyote asivitake achague moja tumuelewe.
Ni kweli mwandishi alitaka kumuona nikki mbishi akibadilika badilika kwenye kuchana katika midundo tofauti tofauti kama ambavyo Weusi hufanya na ndio maana makala yake ikawa na kichwa kisemacho Nikki Mbishi anapaswa kujifunza kutoka kwa weusi. Nahisi mwandishi atakuwa anafarajika kuona angalau ushauri wake umefanyiwa kazi.
Kuna wachanaji wengi leo hii wanachana wanaeleweka ambao wanatamani kuwa kama Nikki Mbishi lakini Nikki mwenyewe anajikataa kama alivyosema kwenye moja ya mistari yake. Napata shida kuelewa kama Nikki mbishi anafata Nyayo zake au anafata nyayo za weusi kama mwandishi alivyoshauri. Najiuliza tu kama anafata nyayo za Weusi, Je hao wanaofata nyayo zake anawaachaje? Au ndio atatimiza neno lake kwamba hawezi kutabiri wala kubashiri wapi ataishia.
Imeandikwa na
Malle Hanzi
O715076444
©2015

No comments:

Post a Comment